Maaskofu nchini DRC waitaka Jumuiya ya Kimataifa kusaidia utekelezwaji wa mkataba wa kisiasa
Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, lililoongoza mazungumzo ya kisiasa kati ya serikali na upinzani na kufikia mkataba, linaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuingilia kati ili kusaidia kutekelezwa kwa mkataba huo.
Imechapishwa:
Kiongozi wa Baraza hilo Askofu Mkuu Marcel Utembi, ameliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa, mkataba huo utatekelezwa kikamilifu ikiwa wataingilia kati na kusaidia kutoa shinikizo za pande zote kuuheshimu.
Wito huu unakuja wakati huu wanasiasa wa serikali na upinzani wakiendelea na mazungumzo ili kukubaliana muundo wa serikali mpya, itakayoongozwa na Waziri Mkuu kutoka upande wa upinzani.
Mapema mwaka huu, Umoja wa Mataifa ulitoa wito kwa pande zote mbili kuuheshimu mkataba huo uliotiwa saini na serikali na upinzani, mwezi Desemba 31 mwaka 2016.
Uchaguzi Mkuu unatarajiwa kufanyika nchini DRC mwisho wa mwaka huu, na rais Joseph Kabila hatarajiwi kuwania kwa mujibu wa mkataba huo.