EU yakosoa uchaguzi wa Gabon, matokeo kutangazwa wakati wowote
Wakati matokeo rasmi ya uchaguzi mkuu uliofanyika mwishoni mwa juma nchini Gabon, yakitarajiwa kutangazwa hii leo, waangalizi wa umoja wa Ulaya wanasema uchaguzi huo ulikosa uwazi huku kukiwa na kasoro nyingi.
Imechapishwa:
Waangalizi hao wamelaani kukosekana kwa uwazi hasa kwa tume ya taifa ya uchaguzi nchini humo, baada ya kushindwa kutoa taarifa muhimu kwa wakati kama vile orodha ya wapiga kura na vituo vilivyotumika kupigia kura.
Haya yanajiri wakati huu mgombea wa upinzani Jean Ping, akiendelea kusisitiza kuwa yeye ndiye mshindi wa uchaguzi wa mwishoni mwa juma, huku akimtaka Rais Ali Bongo kukubali kushindwa.
Serikali imeendelea kukanusha madai ya Ping, ikimtaka aache kutoa matamshi ambayo huenda yakasababisha hali ya sintofahamu.
Msikilizaji wakati fulani nchi ya Gabon ilikuwa mshirika mkubwa wa Serikali ya Ufaransa, ambayo wakati wa vita baridi ilikuwa ikiwafadhili viongozi wala rushwa barani Afrika, uhusiano ambao hivi sasa wataalamu wanasema umeisha.
Antoine Glaser mwanahabari na mwanadiplomasia wa Ufaransa aliyeandika vitabu kadhaa kuhusu uhusiano wa Ufaransa na Gabon, anasema kwa sasa hali ni tofauti na kiongozi yeyote ajaye bado atakuwa hana umiliki wa asilimia mia wa rasilimaliza za nchi hiyo.
Uchaguzi wa mwaka huu umeelezwa kuwa wa ushindani mkubwa zaidi toka ule wa mwaka 2009 uliokumbwa na vurugu.