Pata taarifa kuu
JAPAN-AU-KENYA

Japan yatangaza kutoa Dola za Marekani Bilioni 30 kuyasaidia mataifa ya Afrika

Japan imetangaza kutoa Dola za Marekani Bilioni 30 kusaidia kujenga na kukarabati miundo mbinu, kuimarisha sekta ya elimu na afya barani Afrika.

Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe akiwahotubia viongozi wa Afrika katika mkutano wa maendeleo kati ya Japan na Afrika uliofunguliwa jijini Naieobi nchini Kenya tarehe 27 mwezi Agosti 2016
Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe akiwahotubia viongozi wa Afrika katika mkutano wa maendeleo kati ya Japan na Afrika uliofunguliwa jijini Naieobi nchini Kenya tarehe 27 mwezi Agosti 2016 Reuters
Matangazo ya kibiashara

Tangazo hili limetolewa na Waziri Mkuu wa nchi hiyo Shinzo Abe katika mkutano wa tatu wa Maendeleo kati ya Japan na bara la Afrika (TICAD), ambao umefunguliwa rasmi jijini Nairobi nchini Kenya siku ya Jumamosi.

Abe amesema serikali yake itatoa fedha hizo kwa kipindi cha miaka mitatu ijayo kuanzia mwaka huu ikiwa ni pamoja na Dola za Marekani Bilioni 10 kuanza kujenga na kukarabati miundo mbinu kama barabara, viwanja wa ndege, miradi ya umeme na bandari katika mataifa mbalimbali ya Afrika.

Fedha hizi zitatolewa kupitia Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Viongozi wa Mataifa ya Afrika wakiwa na Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe wakati wa Mkutano mkuu wa maendeleo kati ya serikali ya Japan na bara la Afrika uliofanyika kati ya Agosti 27-28 jijini Nairobi nchini Kenya.
Viongozi wa Mataifa ya Afrika wakiwa na Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe wakati wa Mkutano mkuu wa maendeleo kati ya serikali ya Japan na bara la Afrika uliofanyika kati ya Agosti 27-28 jijini Nairobi nchini Kenya. Reuters

Aidha, Waziri Mkuu Abe amewaambia viongozi wa bara Afrika zaidi ya 30 kuwa, msaada huo unaonesha kiasi gani Japan inaliamini bara la Afrika na watu wake lakini pia nchi yake inaguswa na ina imani na maendeleo yanayopigwa katika  bara hilo.

Msaada mwingine kama huu ulitolewa mwaka 2013, wakati Japan ilipotangaza kutoa Dola za Marekani Bilioni 32 kwa kipindi cha miaka mitano, na hadi mwaka huu wa 2016 asilimia 67 ya fedha hizo zimetumiwa katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Kuhusu Elimu, Japan imesema  itafadhili mafunzo kwa walimu wa masomo ya Hesabu na Sayansi wapatao 20,000 lakini pia itatoa mafunzo kwa wataalaam wengine 20,000 kuhusu namna ya kupambana na magonjwa ya kuambukiza.

Rais wa Chad na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Idriss Derby akizungumza katika mkutano huo, ameitaka serikali ya Japan pia kusaidia mataifa mbalimbali ya Afrika kupambana na ugaidi.

Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe (Kushoto) akisalimiana na rais wa Chad na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika wakati wa Mkutano mkuu wa maendeleo kati ya serikali ya Japan na bara la Afrika uliofanyika kati ya Agosti 27-28 jijini Nairobi nchini Kenya
Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe (Kushoto) akisalimiana na rais wa Chad na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika wakati wa Mkutano mkuu wa maendeleo kati ya serikali ya Japan na bara la Afrika uliofanyika kati ya Agosti 27-28 jijini Nairobi nchini Kenya Reuters

Huu ndio mkutano wa kwanza kuhusu nchi ya Japan na bara la Afrika kufanyika barani Afrika na hususan nchini Kenya.

Mkutano huo unamalizika siku ya Jumapili.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.