Posho kuchelewa yawa kikwazo kwa wanajeshi wa AMISOM, Somalia
Wanajeshi wa umoja wa Afrika walioko nchini Somalia, hawajalipwa posho zao kwa zaidi ya miezi mitano, wakati huu athari za kupunguzwa kwa msaada wa kifedha kutoka nchi za umoja wa Ulaya zikianza kushuhudiwa.
Imechapishwa:
Jumatatu ya wiki hii, umoja wa Ulaya umesema kuwa hadi sasa haujatoa kiasi chochote cha fedha kusaidia tume ya AMISOM nchini Somalia, kwa kile umoja huo unasema ni mchakato wa ndani wa utoaji wa fedha hizo pamoja na ufinyu wa bajeti.
Mkuu wa ujumbe wa umoja wa Ulaya kwenye umoja wa Mataifa, Gary Quince, amesema kuwa uhaba wa fedha ndio sababu ya kuchelewa kulipwa kwa posho hizo na kuongeza kuwa ndio maana msaada huo wa fedha umepunguzwa na hasa kutokana na ufiny wa bajeti kwenye nchi wanachama.
Kuchelewa kulipwa kwa fedha hizi, tayari kumeanza kuathiri shughuli za tume hiyo nchini Somalia, ambapo juma lililopita, Serikali ya Uganda ilitangaza kuwa kuanzia mwakani itaanza kuwaondoa wanajeshi wake kutoka Somalia, kutokana na sababu za kifedha.
Umoja wa Ulaya ndio mfadhili mkuu wa AMISOM nchini Somalia, ambapo inatoa kiasi cha dola za Marekani bilioni 1.2 toka mwaka 2007, ambapo nusu ya fedha hizo ambazo ni dola za Marekani milioni 575 zimekuwa zikutumika kulipa posho kwa wanajeshi, gharama za polisi wa tume hiyo na kulipa mshahara wa wafanyakazi wa kitaifa na kimataifa walioko nchini Somalia.
Mapemwa mwaka huu umoja wa Ulaya ulitangaza kupunguza misaada yake kwa AMISOM kwa asilimia 20.