Wakimbizi kambi ya Daadab, mashakani baada ya UN kukubali ifungwe
Hatimaye Umoja wa Mataifa umeunga mkono juhudi za Kenya za kuwarudisha maelfu ya wakimbizi raia wa Somalia nchini mwao na kuifunga kambi ya wakimbi ya Dadaab ifikapo mwezi November mwaka huu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Uamuzi huu umekuja baada ya rais Uhuru Kenyatta kukutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon, jinini Brussels nchini Ubelgiji.
Kenya imekuwa ikisema itawarudisha nyumbani wakimbizi hao na kuhakikisha kuwa wanaondoka kwa usalama, ikisema sababu yake kuu ni ya kiusalama.
Moon amesema, Umoja wa Mataifa utatafuta fedha ili kuisaidia Kenya kuwarudisha nyumbani wakimbizi hao kwa njia nzuri na ya kibinadamu.
Aidha, amesema kuwa ameelewa sababu zilizotolewa na Kenya kuamua kuwarudisha nchini Somalia wakimbizi hao lakini pia akaishukuru serikali kwa kuwapa hifadhi wakimbizi hao kwa zaidi ya miaka 20.
Hatua za mwisho yza kuwaondoa wakimbizi hao nchini Kenya, zitajadiliwa mwezi ujao pembeni mwa mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu biashara na maendeleo utakaofanyika jijini Nairobi mwezi ujao.
Kenya inasema, gharama ya kuwarudisha nyumbani wakinbizo hao itaigharimu Shilingi za nchi hiyo Bilioni 11 na hadi sasa imefanikiwa kupata tu Shilingi Milioni 720.
Wanaharakati wa haki za binadamu wamekosoa mpango wa Serikali ya Kenya wa kuifunga kambi ya Daadab, na kuhoji utaratibu ambao utatumiwa na hautakiuka haki za binadamu.