UNHCR yatiwa wasiwasi na ongezeko la wakimbizi
Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Wakimbizi duniani la (UNHCR) limesema takribani alfu ishirini na tano wa Nigeria, wamekimbilia kaskazini mwa Cameroon mwishoni mwa wiki iliyopita kufuatia mapigano kati ya jeshi la serikali na kundi la kigaidi la Boko Haram.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Msemaji wa UNHCR katika eneo la Afrika magharibi ameliambia shirika la habari la Ufaransa AFP kuwa shirika hilo linashirikiana na serikali ya Cameroon ili kuwahamishia wakimbizi hao mbali na maeneo ya mapigano na kuwapatia chakula pamoja na huduma za maji na afya.
Hata hivyo UNHCR imesema kwamba haiwezi kufikia maeneo ya mpakani kwa sababu mapigano yanaendelea pia kwa upande wa Cameroon.
Adrian Edwards msemaji wa UNHCR amedokeza kuwa misafara ya wahamiaji kutoka mpakani hadi Kousseri imeanza Alhamisi wiki hii ikihamisha wakimbizi 2,000 kila siku.
UNHCR inakadiria kwamba idadi ya wakimbizi nchini Cameroon ni takriban 66,000, wengine 18,000 wakiwa wametafuta hifadhi nchini Chad, na wengine milioni moja wakiwa ni wakimbizi wa ndani kaskazini mwa Nigeria.