Mauaji ya Yebei yaendelea kuzua hisia tofauti Kenya
Maswali zaidi yameendelea kuibuka kuhusu mauaji ya kikatili yaliyotekelezwa dhidi ya Meshack Yebei, shahidi muhimu katika kesi inayomkabili naibu rais wa Kenya William Ruto kwenye mahakama ya ICC.
Imechapishwa:
Meshack aliuawa mwezi Desemba mwaka uliopita na mwili wake ulipatikana mwishoni mwa juma lililopita huku ukiwa umekatwakatwa kwa mapanga, jambo ambalo upande wa utetezi unadai alikuwa shahidi wao muhimu.
Hata hivyo Jumatano ya wiki hii, wabunge wa vyama vinavyounda serikali ya Jubilee, wametaka kukamatwa kwa mwanaharakati, Ken Wafula wanayedai kuwa huenda akawa amehusika kwenye mauaji ya shahidi huyo.
Hata hivyo mwanaharakati huyo, amesisitiza kumfahamu shahidi huyo na kudai kuwa upande wa utetezi ulikuwa umemuahidi kumpa kiasi cha fedha ili atoe ushahidi kwa upande wa naibu wa rais lakini haikuwa hivyo.
Tayari ofisi ya mwendesha mashtaka mkuu wa Kenya imeagiza polisi kufanya uchunguzi kubaini sababu na watu waliohusika na mauaji ya shahidi huyo.